MASHINDANO ya kutafuta wasichana warembo yalianza nchini mwaka 1960 wakati huo Tanzania Bara ikiitwa Tanganyika. Wasichana warembo walitafutwa katika maeneo machache tu na hayakuwa na sura ya kitaifa kama ilivyo sasa.
Shindano la kwanza la kumtafuta Miss Tanzania lilifanyika mwaka 1967 katika Hoteli ya Kilimanjaro jijini Dar es Salaam,Theresia Shayo akatwaa taji hivyo kuwa Miss Tanzania wa kwanza.
Mwaka huo huo,Serikali iliyapiga marufuku mashindano hayo kwa kile ilichodai kuwa yalikiuka maadili na utamaduni wa Tanzania.
Mwaka 1994 serikali chini ya utawala wa Rais wa Awamu ya Pili, Ali Hassan Mwinyi iliruhusu mashindano hayo,Kamati ya Miss Tanzania chini ya uongozi wa Hashimu Lundenga ilichukua jukumu la kuandaa shindano hilo.
Mwaka 1994 Aina Maeda alitwaa taji la Miss Tanzania,na tangu wakati huo mashindano hayo yalianza kupata sura ya kitaifa,na yenye hadhi.
Mwaka uliofuata ilikuwa ni zamu ya mrembo kutoka Dodoma, Emily Adolf,akawa Miss Tanzania wa pili, Shose Senare aliibuka kuwa mrembo wa Tanzania mwaka 1996.
Mwaka 1997 mrembo wa Arusha, Saida Kessy, alitwaa taji la Miss Tanzania na ameweka rekodi ya kuwa mrembo wa kwanza Tanzania kupewa zawadi ya gari.
Mwaka 1998,Basila Mwanukuzi,alifuata nyayo za Saida,mwaka uliofuata ilikuwa ni zamu ya Hoyce Temu alipoiwakilisha wilaya ya Ilala.
Nyota ya Ilala iling'ara tena mwaka 2000 wakati Jacqueline Ntuyabaliwe alipotwaa taji la Miss Tanzania, mwaka uliofuatia ilikuwa ni zamu ya wilaya ya Temeke.Mwaka 2002 Angela Damas alilirudisha taji hilo Ilala,Sylvia Bahame akaiwezesha Temeke kuipata tena heshima hiyo.
Kuanzia mwaka 2004 Wilaya ya Kinondoni ilitawala shindano la Miss Tanzania kwa kutwaa taji hilo mfululizo kwa miaka minne. Miss Tanzania mwaka huo alikuwa Faraja Kotta,akafuatiwa na Nancy Sumari mwaka 2005.
Wema Sepetu,aliibuka kuwa Miss Tanzania mwaka 2006,Richa Adhia alihitimisha utawala wa Wilaya hiyo mwaka 2007 kwa kuwa mwaka uliofuata mrembo wa Tanzania, Nasreem Karim alitoka nje ya Dar es Salaam.
Zawadi kwa washindi zimekuwa zikiongezeka mwaka hadi mwaka sanjari na thamani, ikiwa ni pamoja na kiwango cha bei ya gari analopata mshindi wa kwanza, na fedha taslimu.
Miss Tanzania 2009 atapata zawadi ya gari aina ya Suzuki Grand Vitara lenye thamani ya shilingi milioni 53 , fedha taslimu shilingi milioni tisa. Mshindi wa pili atapata fedha taslimu shilingi milioni sita na laki mbili na mshindi wa tatu atapata shilingi milioni nne.
Zawadi hizo ni nyongeza ya nyingine alizopata aliposhiriki mashindano ngazi za chini kuanzia kwenye kitongoji hadi akaata nafasi ya kushiriki fainali ya kumsaka Miss Tanzania.
Licha ya zawadi hizo, Miss Tanzania 2009 ataliwakilisha taifa katika shindano la Kimataifa la Miss World.
Hadi sasa Kanda ya Kinondoni imeonyesha kuwa ndio chemchem ya malkia wa urembo nchini kwani tayari inayo warembo wanne wamewahi kunyakua taji la Miss Tanzania na hivyo kufanya kanda hiyo kuwa tishio katika fainali za mashindano hayo.
Mbali na zawadi za kifahari ambazo washindi wamekuwa wakipewa lakini imekuwa pia ni njia ama mlango kwa warembo wengi walioshiriki shindano hilo na ushuhuda upo maana wengi wao hivi sasa wamepata nafasi za uongozi katika taasisi mbalimbali.
Baadhi yao wamepata ajira, wengi wao wakiwa ni maofisa uhusiano katika taasisi mbalimbali akiwemo mshindi wa Pili wa shindano la Miss Tanzania 1994 Tabasamu Ngongoseke ambaye sasa anajulikana kama Lucy Kihwele.Awali,Lucy alikuwa Ofisa Uhusiano wa kampuni ya MultiChoice Tanzania baadaye alihamia benki ya Standard Charted.
Miss Tanzania 1996 Shose Sinare ni Mkuu wa Huduma za Kibenki katika Benki ya Stanbic Tanzania.
Si hivyo tu, mashindano ya Miss Tanzania pia yamewawezesha warembo kuwa wajasiriamali wakiwemo,Irene Kiwia na Nancy Sumari.
Irene alikuwa Miss Temeke mwaka 1999, na alifanikiwa kuwa miongoni mwa warembo 10 bora katika shindano la Miss Tanzania.
Miss Tanzania 20
Miss Tanzania mwaka 2005,Nancy Sumari, na Irene wameanzisha shindano la kitaifa kuwasaka mabinti kwa ajili ya kuwa wanamitindo liitwalo,Kisura wa Tanzania.
Msichana kutoka Arusha,Emmy Melau, alifanikiwa kuwa mshindi wa kwanza wa shindano hilo,amepata mkataba wa kufanya kazi za mitindo nchini Afrika Kusini.
Shindano la Miss Tanzania pia limemuwezesha mrembo wa nchi hii mwaka 2001, Happiness ‘Millen’ Magesse kuwa mwanamitindo, kwa sasa ni kati ya wanamitindo bora Afrika, anafanya kazi Afrika Kusini. .
Tanzania haijawahi kutwaa taji la Miss World, lakini Miss Tanzania mwaka 2005, Nancy Sumari,alinyakua taji la Miss World Afrika,kabla ya hapo hakuna mrembo wa Tanzania aliyewahi kufikia mafanikio hayo na hadi sasa rekodi hiyo haijavunjwa. |